Jumatatu, 24 Juni 2013

Brazil yazidi kusonga mbele Kombe la Mabara


Mshambuliaji wa Italia, Mario Balotelli (kushoto) akizuiwa na beki wa Brazil, David Luiz wakati wa mechi ya Mabara kwenye Uwanja wa Fonte Nova mjini Salvador. Picha AFP.  

Brazil. Timu ya taifa ya Brazil juzi imeichapa Italia 4-2 katika mashindano ya Kombe la Mabara na hivyo Brazil kumaliza hatua ya makundi ikiongoza kundi A.
Mshambuliaji Neymar wa Brazil katika mechi hiyo alifunga bao na hivyo kufikisha mabao matatu katika mashindano hayo.
Brazil ilipata bao la kwanza mwishoni mwa kipindi cha kwanza ambalo lilifungwa na Dante, lakini Italia ilisawazisha bao hilo katika dakika ya 51 mfungaji akiwa Emanuele Giaccherini.
Katika dakika ya 55, Neymar aliifungia Brazil bao la pili baada ya kupiga mpira wa adhabu uliokwenda moja kwa moja nyavuni na kumuacha kipa mahiri wa Italia, Gianluigi Buffon asijue la kufanya.
kama hiyo haitoshi Brazil ilipata bao la tatu katika dakika ya 66 ambalo lilifungwa na Fred, lakini Italia nao hawakubaki nyuma kwani katika dakika 71 walifunga bao la pili ambalo lilifungwa na Giorgio Chiellini.
Katika dakika ya 80 bado kidogo Italia wangesawazisha hata hivyo mpira wa kichwa uliopigwa na Christian Maggio ulipita juu kidogo ya goli. Pia dakika chache baadaye Mario Balotelli naye alipiga shuti kali, lakini lilitoka nje.
Ilipofika dakika ya 89, Brazil ilijihakikishia ushindi wa mechi hiyo kwani Fred alitumia vizuri mpira uliopanguliwa na kipa wa Italia na hivyo kuiandikia Brazil bao la nne.
Brazil imemamaliza hatua hii ya makundi ikiwa na pointi tisa ikiwa na pointi tatu juu ya Italia inayomfuatia huku timu za Mexico na Japan zikitolewa mashindanoni.
“Brazil ipo tayari kwa ajili ya mechi ya nusu fainali, tumefanikiwa kusonga mbele kwa sababu ya ufundi mzuri na mbinu bora, pia kikosi kinajiamini,”alisema kocha wa Brazil, Luiz Felipe Scolari.

0 maoni:

Chapisha Maoni

Share

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More