Alhamisi, 11 Aprili 2013

KADA WA CHADEMA AZIDI KUTESWA

JESHI la Polisi Makao Makuu limeendelea kumshikilia kwa siku 11 bila kumfikisha mahakamani Mwenyekiti wa Baraza la Vijana la CHADEMA (BAVICHA) mjini Bukoba, Evodius Justinian (30) huku ndugu zake wakizuiliwa kumpa chakula isipokuwa maji tu.
Justinian alishikiliwa mjini Bukoba Aprili 2, mwaka huu kisha kusafirishwa hadi jijini Mwanza na kuhojiwa, kisha Dar es Salaam huku akipewa mateso makali ya kulazimishwa akubali kuhusika kutengeneza video inayomhusisha na uchochezi Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa CHADEMA, Wilfred Lwakatare.
Awali ndugu zake na viongozi wa CHADEMA mjini Bukoba walielezwa na polisi kuwa Justinian anasafirisha kwenda wilayani Igunga, Tabora ambako alidaiwa kuwa alitenda makosa ya jinai, lakini alifichwa jijini Mwanza.
Wakizungumza na gazeti hili, mawakili wa mtuhumiwa huyo Nyaronyo Kicheere na Peter Kibatala walisema kuwa juzi jioni ndugu zake walimpelekea chakula, lakini walipofika waliambiwa kuwa haruhusiwi chakula isipokuwa maji tu.
“Asubuhi alipelekewa chai, lakini polisi walidai kuwa ndugu walichelewa na hivyo kuwazuia. Na walipopeleka chakula cha mchana waliambiwa hayupo kwani alikuwa amepelekwa hospitali bila kuitaja kwa jina,” alisema Kicheere.
Kicheere aliongeza kuwa baada ya ndugu kuwapa taarifa hiyo, yeye na wakili mwenzake Kibatala walilazimika kuondoka mahakamani Kisutu walipokuwa wakimsubiri mteja wao afikishwe.
Mawakili hao walisema wanakusudua wakati wowote kupeleka maombi Mahakama Kuu kudai polisi wapeleke mwili wa mtuhumiwa mahakamani (habeas corpus).
Lakini pia mawakili hao walisema kuwa leo wataendelea kushinda mahakamani muda wote wa kazi kumsubiri mteja wao.
Waliwataka Watanzania wakiwemo wanasheria na watetezi wa haki za binadamu kuendelea kupiga kelele dhidi ya Jeshi la Polisi linavyokiuka haki za binadamu.
Akizungumzia hatua ya mtuhumiwa huyo kutofikishwa mahakamani kama ilivyokuwa imeahidiwa, Msemaji wa Jeshi la Polisi, Advera Senso alisema wakiwa tayari watasema na kuomba watu wasiingilie kazi yao.
“Tutasema siku ya kumfikisha, hapa suala la msingi ni polisi tunafanya nini, ni kama wewe unavyoandika habari, hakuna wa kukuuliza,” alisema Senso.
Alipoelezwa juu sheria inavyotaka mtuhumiwa kufikishwa mahakamani ndani ya saa 24 baada ya kukamatwa, Senso alisema pasipo kufafanua kuwa sheria hiyo hiyo inaweza kutumika vinginevyo.
Jumatatu wiki hii, mbele ya wakili wake Kicheere, mtuhumiwa huyo alieleza unyama aliofanyiwa na jeshi hilo wakati wote wa mahojiano mkoani Mwanza na jijini hapa.
Katika maelezo yake yaliyoshuhudiwa na Ofisa wa Polisi Makao Makuu, Advocate Nyombi, Justinian alisema kuwa baada ya kutolewa mjini Bukoba kwa siri bila ndugu zake kujua, alipelekwa jijini Mwanza na kuhojiwa bila kuruhusiwa kuonana na wakili wake.
Alieleza kuwa wakati wote wa mahojiano hayo alikuwa akilazimishwa kukiri kurekodi video ya Lwakatare inayoonesha mikakati ya ugaidi.
Alisema alisafirishwa kwa siri kwa ndege hadi Dar es Salaam, akapelekwa chooni na kupigwa, kutishiwa na kuteswa kwa nyaya za umeme na kunyimwa fursa ya kupewa chakula.
“Nimepigwa na polisi nikiwa Mwanza, nikiwa chooni Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam wakati naletwa huku, polisi wakaniambia mimi ni mtu hatari sana, niseme nilifanya nini Igunga.
“Nikiwa Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam niliomba kwenda chooni, waliingia pamoja na mimi wakanipiga sana, nimeshaandika maelezo kwa kulazimishwa, niliomba kuwa na wakili wakanikatalia,” alisema.
Aliongeza kuwa akiwa Dar es Salaam alihojiwa aseme ukweli kuhusu video ya Lwakatare. Akawajibu kuwa ilifanyiwa uhariri na Ludovick, lakini akapigwa makofi na askari wakaagiza nyaya za umeme za kutesea.
“Waliposema kuleta nyaya za umeme, kwa kuhofia mateso ya umeme nikasema hii video ni yangu,” alisema.

0 maoni:

Chapisha Maoni

Share

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More