Jumapili, 7 Aprili 2013

Tanzania kupigana vita Congo DRC

 

Dar es salaam. Tanzania itapeleka kikosi cha askari 850 kwa ajili ya kupambana na waasi wa Kundi la M23 katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) ikiwa ni utekelezaji wa Azimio la Umoja wa Mataifa.
Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa wiki iliyopita lilipitisha azimio namba 2098 linalotaka kupelekwa kwa jeshi la kukabiliana na vikundi vya waasi mashariki mwa Congo.
Msemaji wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Kanali Kapambala Mgawe alisema kikosi kiko katika maandalizi kwa ajili ya operesheni hiyo.
“Tuko tayari. Wanajeshi wetu 850 wako tayari na wakati wowote kuanzia sasa wataanza safari ya kuelekea Congo kwa ajili ya kushiriki operesheni hiyo,” alisema alisema Kanali Mgawe.
Kikosi hicho kitaungana na vikosi vya nchi nyingine kutoka nchi za Afrika Kusini, Msumbiji na Malawi kwa ajili ya operesheni hiyo.
Kanali Mgawe alisema kuwa jambo linalosubiriwa sasa ni Umoja wa Mataifa kupanga siku ya kuanza kwa operesheni hiyo. Umoja wa Mataifa ndiyo unatakiwa kugharimia kazi hiyo ya kufutilia mbali makundi yenye silaha, ambayo yamekuwa yakisumbua kwenye eneo hilo la Mashariki mwa Congo.   
Taarifa kutoka New York zinasema kuwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilikutana jana na kisha kuidhinisha mpango wa kutumwa askari 3100. Jeshi hilo linatakiwa kuweka kambi katika Mji wa Goma, ambao uko katika Jimbo la Kivu ambalo ndiyo kitovu cha uasi wa M23.
Kikosi hicho cha Umoja wa Mataifa kitakuwa na batalioni tatu. Moja ya kupigana vita, kingine kwa ajili ya kutungua ndege na kingine kitaundwa na majasusi wa kuchunguza nyendo za waasi hao.
Eneo la Mashariki la Congo limekuwa halina amani kutokana na kuibuka vikundi vya waasi mara kwa mara na hivi sasa kilichoshika kasi ni kile cha M23. Ripoti ya Umoja wa Mataifa iliyotolewa hivi karibuni ilizituhumu nchi za Rwanda na Uganda kuwa zinaunga mkono waasi hao. Nchi hizo, hata hivyo, zimepinga tuhuma hizo.
Hii itakuwa mara ya pili kwa Tanzania kupeleka vikosi vyake kupigana vita ili kurudisha amani katika nchi, iliwahi kufanya hivyo mwaka 2008 ilipopeleka batalioni moja ili kukikomboa Kisiwa cha Anjouan kilichokuwa kimejitenga na Comoro. Ilikuwa ni utekelezaji wa Azimio la Umoja wa Afrika (AU).

 

0 maoni:

Chapisha Maoni

Share

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More