Ijumaa, 3 Mei 2013

Hali halisi kiuchumi:Umaskini na maisha bora uswazi


Baadhi ya nyumba za watu wanaoishi Manzese jijini Dar es Salaam .
Katika duka moja, Manzese Midizini, sukari, majani ya chai na chumvi vimefungwa katika paketi zenye ujazo unaofanana (sawa)  na ule wa paketi za karanga. Kila paketi moja ina bei yake.
Sukari inauzwa Sh150 wakati majani ya chai na chumvi vinauzwa kwa bei ya Sh50 kiwango ambacho kinaelezwa kwamba  wakazi wengi wa eneo hilo wanamudu kununua.
Wakazi wengi wanaonunua bidhaa hizo katika bidhaa ndogo ni wale wa kipato cha chini ambao wanaishi chini ya dola moja.
Hii ndio Manzese kiuchumi
Muuza duka anayejitambulisha kwa jina la Issaya Mushi anasema anafunga bidhaa hizo katika ujazo huo kwa sababu wateja wake wengi hawana uwezo wa kununua katika kiwango cha robo kilo, nusu au kilo moja na kuendelea.
“Kwa siku unaweza kupata mteja mmoja au wawili wa nusu kilo na kwa mwezi wastani wa wateja wanne wa kilo nzima,” anasema Mushi. Anabainisha kuwa hali kama hiyo ipo pia katika vipimo vya bidhaa nyingine kama vile mafuta ya taa, mafuta ya kupikia, na mchele.
“Mchele wa Sh2,000 huku utamuuzia nani? Watu wananunua mchele unaouzwa chini ya bei hiyo. Watu wananunua  mchele ambao uko kwenye kipimo cha nusu kilo au nusu na robo,” anasema
Wakazi hao ni sehemu ya maelfu ya watu nchini ambao wanaishi katika lindi la umaskini wa kipato. Kutokana na hali hiyo ya umaskini unasababisha  watu hao washindwe  kumudu gharama za maisha kwa mfano gharama za chakula, usafiri, na gharama nyingine.
Gharama hizo ni pamoja na michango ya mshahara wa mlinzi ambao ni wastani wa Sh500 kwa kila mtoto au watoto wanaosoma,  fedha za tuisheni, mitihani ya majaribio na huduma nyingine wanazolazimika kulipia katika shule wanazosoma watoto wao kuanzia zile za msingi hadi sekondari za Kata na gharama za matibabu.
Takwimu za kiuchumi za Tume ya Taifa ya Takwimu (NBS), zinabainisha  kwamba mfumuko wa bei umedhibitiwa mpaka kufikia asilimia 11.1 katika Machi, mwaka huu ukilinganisha na kasi ya ukuaji Februari, mwaka huu, lakini hali hiyo haijabadili chochote kwa wakazi hao.
Upande mwingine imeelezwa kwamba Pato la Taifa limekua likiongezeka hivi karibuni, lakini umaskini wa kipato kwa wananchi unaendelea kuwatafuna kwa kuwa Pato la Taifa linakua kitakwimu kuliko hali halisi.
Watu 100, 36 kati yao ni maskini
Takwimu za hivi karibuni za Mpango wa Taifa wa Kukuza Uchumi na Kupambana na Umaskini (Mkukuta), zinabainisha kwamba  Watanzania 100 kati yao,  36 wanaishi katika umaskini wa kipato na kiwango hicho cha umaskini kimetofautiana kutoka eneo moja hadi lingine katika maeneo ya mijini na vijijini.
Taarifa ya Benki ya Dunia (WB) ya hivi karibuni  inaonyesha  katika kipindi cha miaka 30 iliyopita, kumekuwapo na maboresho makubwa ya hali ya maisha ya watu wengi duniani kiasi kwamba kiwango cha umaskini katika ngazi ya dunia kimepungua.
Ripoti hiyo inabainisha kwamba kiwango cha umaskini kinaweza kupungua kwa ujumla, lakini bado kuna baadhi ya nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara Tanzania ikiwamo,  watu wake wanaishi katika umaskini mkubwa.
Kulingana na takwimu hizo, zaidi ya watu bilioni moja duniani wanaendelea kuishi katika umaskini wa kipato na hiyo ni changamoto kwa viongozi wa nchi husika.
Kutokana na hali hiyo, viongozi wa nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara Barani Afrika wanapaswa kuweka mikakati kufikia  dira na mipango ya Umoja wa Mataifa ya kupunguza umaskini wa kipato katika ngazi ya familia ifikapo mwaka 2030.
Ripoti ya Benki ya Dunia imeonyesha kwamba Tanzania pamoja na uwapo wa amani na kuwa ya pili  kwa uchumi mkubwa, ina idadi kubwa ya watu wanaoishi katika umaskini wa kutisha kulinganisha na nchi zingine za Afrika Mashariki.
Ripoti hiyo inabainisha  kwamba  watu wanaoishi katika umaskini Tanzania ni asilimia 68 wakati Uganda ni asilimia 38, Kenya asilimia 43, Rwanda 63 na Afrika Mashariki inatajwa kuwa nyuma katika kuelekea kufikia malengo ya milenia  mwaka 2015.
Kulingana na malengo hayo ambayo Tanzania na  nchi  nyingine 89 zimeridhia ni pamoja na kutokomeza umaskini uliokithiri.
Profesa Ibrahim Lipumba ambaye ni mchumi na Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (Cuf), anasema dhana ya maendeleo kwa watu wote inasisitiza kila mtu kushiriki au kushirikishwa ili anufaike na kujivunia maendeleo ya nchi yake.
“Robo tatu ya Watanzania wanaishi vijijini na kutegemea kilimo, naamini mapinduzi katika kilimo yataongeza tija na uzalishaji nchini.  Pia ongezeko la uzalishaji wa chakula litapunguza mfumuko na kushusha gharama za chakula Tanzania,” anasema Profesa Lipumba.
Anabainisha kuwa lishe bora na ya kutosha itasaidia kupunguza utapiamlo na kuboresha afya za wananchi na kuongeza uzalishaji mkubwa wa mazao ya kilimo  nchini. Profesa Lipumba anataka matumizi mazuri ya raslimali ili kuleta tija tarajiwa kwa wananchi wote badala ya kuwa kama ilivyo sasa.
Umaskini unasababisha haya?
Umaskini wa kipato unachangia mambo mengi ambayo ni pamoja na vifo kwa watoto chini ya miaka mitano vinavyotokana na utapiamlo, maambukizi ya Ukimwi, uhalifu, umalaya na watu kupoteza maisha kutokana na kushindwa kumudu huduma za matibabu.
Wakati hali halisi ya kiuchumi ikiwa hivyo kwa wakazi wa Manzese na maeneo mengine yanayofanana na eneo hilo kwa mfano Tandika, Buguruni, na Tandale, wakazi wa mikoani ambao wanaishi chini ya dola moja wamekuwa katika wakati mgumu na wengine wamekuwa wakilazimika kula mizizi inapotokea tatizo la njaa.
Serikali ina wajibu wa kuhakikisha inachukua hatua za makusudi kukabili hali hiyo na kubadili maisha ya Watanzania tofauti na ilivyo hivi sasa. Mambo hayo yakifanyika yatasaidia kuelekea katika maelengo ya milenia ya mwaka 2015.

CHANZO: Mwanachi

0 maoni:

Chapisha Maoni

Share

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More