Jumatano, 1 Mei 2013

Rais Kikwete aunga mkono hoja ya Mbatia kuhusu mitalaa ya elimu

Mbeya. Rais Jakaya Kikwete amekubaliana na hoja ya Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia kuhusu kufanyiwa marekebisho kwa mitalaa ya elimu nchini ili iendane na viwango vya elimu inayohitajika.
Rais Kikwete alisema hayo jana alipokuwa akizungumza na wenyeviti na wamiliki wa shule na vyuo vya binafsi kwenye Ukumbi wa Benjamin Mkapa, Mbeya.
Katika kikao cha Tano cha Bunge, Januari mwaka huu, Mbatia aliwasilisha hoja binafsi kuhusu ubovu wa elimu na mitalaa, hoja aliyodai kufinyangwa na Bunge kabla ya kupatiwa majibu stahiki na hata kuzua mjadala mkali miongoni mwa wadau wa sekta hiyo.
Akizungumza jana, Rais Kikwete alisema: “Mitalaa na mihutasari ya elimu itarekebishwa ili kuzingatia mazingira ya sasa ya dunia na ni lazima tuwe na viwango vya elimu vya kimataifa.”
Rais ambaye alizipongeza shule binafsi kwa kufanya vizuri mara kwa mara, pia aligusia Sera ya Elimu na kusema inaendelea kufanyiwa kazi pamoja na kuimarisha idara za ukaguzi wa shule ili kuepuka kushuka kwa viwango vya elimu.
Awali, katika risala yao, wadau hao wa elimu walilalamikia kodi mbalimbali zinazotozwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), wakisema ndicho chanzo cha wao kupandisha ada kila mwaka pamoja na mitalaa isiyo na vigezo.Mwenyekiti wa Shirikisho la Wamiliki wa Shule na Vyuo, Mahamoud Mringo alisema: “Mwaka jana shule 40 zilifungwa kutokana na kuelemewa na mzigo wa kodi mbalimbali na mwaka huu idadi hiyo inaweza kufikia 100.”
“Tunaiomba Serikali ituondolee kodi ya mshahara (Paye)... tutashindwa kuendesha shule kama tutabanwa kupandisha ada. Serikali inatubana kupandisha ada, lakini papo hapo inatubana kwenye kodi, kwa hapa hatuwezi kuendesha shule, lazima tuongeze ada.”
Leo Rais Kikwete anatarajiwa kuzungumza na wafanyakazi wa Tanzania kwenye kilele cha Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) Uwanja wa Sokoine.

CHANZO: Mwananchi

0 maoni:

Chapisha Maoni

Share

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More