Alhamisi, 23 Mei 2013

Wizi na uharibifu wa muda mrefu wa miundombinu ya umeme TANESCO - waziri wa Nisati na Madini Tanzania

Dodoma. Shirika la Umeme nchini (Tanesco), limepata hasara ya Jumla ya Sh966.18 milioni kutokana na wizi na uharibifu wa miundombinu katika mikoa mbalimbali nchini, Bunge lililezwa jana.
Kauli hiyo ilitolewa na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo wakati akiwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa wizara hiyo kwa mwaka 2013/14.
Waziri huyo alisema, kiasi hicho ambacho ni sawa na Dola za Marekani 603,862 kilipotea katika kipindi cha Julai 2012 hadi Aprili 2013 ambapo ni hasara kubwa zaidi kwa Tanesco.
Kwa taarifa, ni wazi kuwa Tanesco imekuwa ikipata hasara ya karibu Sh96.7 milioni kila mwezi kiasi ambacho ni kikubwa.
“Wizi na uharibifu wa muda mrefu wa miundombinu ya umeme kwa muda mrefu umekuwa ni tatizo sugu kutokana na wahusika kubuni njia mbalimbali za kufanya uharibifu huo na kuisababishia Tanesco na nchi kwa ujumla hasara kubwa,” alisema Muhongo.
Akizungumzia tatizo la kukatika kwa umeme mara kwa mara, alisema, “Tatizo la kukatika kwa umeme ni uchakavu wa miundombinu ya usambazaji na vifaa vyake pamoja na kuzidiwa uwezo kwa mifumo yake.”
Kingine alitaja kuwa ni wizi wa nyaya za shaba na mafuta ya transfoma zaidi kwenye mikoa ya Arusha,Kilimanjaro na Mkoa wa Tanga.
Alitaja mkakati wa kukabiliana na tatizo hilo kuwa ni pamoja na kubadilisha nguzo zilizoharibika katika njia za msongo wa Kv 0.4 na Kv 11 na 33, kukata miti na kubadilisha vikombe vilivyovunjika na nyaya chakavu.
Waziri alitaja miradi mingi ya umeme ambayo wizara inajiandaa kuikamilisha katika maeneo mbalimbali nchini kuwa itagharimu fedha nyingi.
Miradi hiyo ni ile ya MCC, REA ambayo inaendelea kuzinduliwa katika maeneo tofauti na mingi imetekelezwa kwa kiwango cha kuridhisha.
Kwa upande wao Kambi ya Upinzani waliitaka Wizara ya Nishati na Madini kueleza ukweli kuhusu mgao wa umeme ambao unaendelea kuwatesa Watanzania huku kukiwa na taarifa kuwa hakuna mgao.
Akiwasilisha maoni ya kambi hiyo, Msemaji wa Upinzani katika Wizara ya Nishati na Madini,John Nchimbi aliituhumu Serikali kuwa imekuwa ikikanusha kuhusu mgao huo wakati hali ni tofauti na kauli ya Serikali.

0 maoni:

Chapisha Maoni

Share

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More