Jumanne, 14 Mei 2013

Kitendo cha kula Moyo Syria chalaaniwa


Kanda ya video ambayo inaonekana kuonyesha muasi mmoja nchini Syria akila Moyo wa mwanajeshi aliyefariki, imelaaniwa vikali.
Shirika la Marekani la kutetea haki za binadamu, Human Rights Watch, limemtaja muasi huyo kama Abu Sakkar, muasi anayejulikana sana kutoka mji wa Homs, na kusema kuwa vitendo vyake ni vya uhalifu wa kivita.
Chama rasmi cha upinzani nchini Syria kimsema kuwa mshukiwa huyo lazima atakabiliwa na kesi mahakamani.
Kanda hiyo ambayo haiwezi kuthibitishwa , imeonyesha akikata moyo wa mwanajeshi huyo na kuula.
"naapa kwa Mungu, tutakula mioyo yenu na figo zenu , nyinyi wanajeshi wa Bashar,'' alisema muasi huyo akimtaja rais Bashar al-Assad wakati akiwa kando ya maiti ya mwanajeshi huyo.
Shirika la Human Rights Watch, linasema kuwa Abu Sakkar ni kiongozi wa kundi linalojulikana kama Omar al-Farouq Brigade.
"ukataji wa miili ya maadui ni uhalifu wa kivita, lakini la kuudhi zaidi ni swala la ghasia na vita kukithiri,'' alisema Peter Bouckaert wa shirika la HRW.
HRW limesema kuwa,wanaofanya uhalifu kutoka pande zote, lazima wajue kuwa watawajibishwa.
Aidha shirika hilo limesema kuwa Abu Sakkar aliwahi kunaswa kwa kanda ya video akirusha makombora katika maeneo yenye madhehebu ya Shia nchini Lebanon na kisha kusimama kando ya maiti ya wanajeshi waliouawa katika mashambulizi ya kuvizia.
Kanda hiyo iliyowekwa kwenye mtandao siku ya Jumapili, ni moja ya video inazoonyesha picha mbaya zaidi kuwahi kuonyeshwa tangu kuanza kwa vita vya Syria miaka miwili iliyopita.
Umoja wa mataifa unasema kuwa watu 70,000, wameuawa tangu kuanza mapinduzi ya kiraia dhidi ya utawala wa Rais Bashar al-Assad Machi 2011, ingawa baadhi ya mashirika yanasema idadi hiyo imefika watu 80,000.

0 maoni:

Chapisha Maoni

Share

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More