Jumatano, 1 Mei 2013

Ushindani:CCM iko hai au hoi?


Morogoro. Chama Cha Mapinduzi kinaendelea kujitathmini kwa kuwatembelea wananchi na wanachama wake kuangalia uhai wa chama na kukagua utekelezaji wa Ilani yake ya 2010-2015.
Ziara zinaongozwa na Katibu Mkuu, Abdulrahman Kinana ambaye wiki iliyokwisha alimaliza ziara ya siku nane katika Mkoa wa Morogoro.
Morogoro ni mkoa sita kutembelewa na Kinana, tangu alipoteuliwa kushika wadhifa huo Novemba mwaka jana. Tayari amefanya ziara ya namna hiyo katika mikoa ya Mtwara, Rukwa, Geita, Arusha na Kigoma.
Akiwa Morogoro, Kinana alitembelea wilaya sita zinazounda mkoa huo – Kilosa, Kilombero, Ulanga, Gairo, Mvomero, Morogoro Vijijini na Morogoro Mjini.
Uhai wa chama
Morogoro ni miongoni mwa ngome zinazotegemewa na CCM kwani majimbo yote 10 ya uchaguzi yaliyopo katika mkoa yanashikiliwa na CCM. Pia kati ya kata 181 zilizopo mkoani humo, ni chache tu zinazoshikiliwa na vyama vya upinzani.
Hata unapopita katika maeneo mbalimbali ya mkoa wa Morogoro, bendera za kijani zinatawala huku bendera chache za Chadema na CUF zikiwa zinaonekana kupepea.
Katika mkoa huo, Kinana amefungua mashina ya wakereketwa 50 kwa niaba ya mengine zaidi ya 400. Katika mashina hayo, kila shina lilikuwa na idadi ya wanachama wapya kati ya 30 na 70.
Ingawa takwimu halisi za wanachama wapya katika mkoa huo bado hazijapatikana lakini kuna wananchi wengi wamejiunga na chama hicho.
CCM inaonyesha imebadili mbinu ya siasa zake kwa kuyafanya mashina kuwa vikundi vya kujiendeleza kiuchumi badala kuwa vijiwe vya kupika majungu.
Hata risala alizosomewa katika mashina hayo, vijana wakereketwa walielezea miradi wanayoifanya na Kinana akawaongezea ahadi za kuwasaidia ili waweze kufanikisha miradi hiyo.
Kinana anasema vijana ni lazima wawe na mawazo ya kujitegemea kwa kuanzisha miradi mbalimbali ndipo Serikali inaweza kuwasaidia. “Ninapokutana na vijana ambao wamejikusanya na kuanzisha mradi kwa lengo la kujiajiri ninafarijika kuchangia fedha ili kuwaongezea nguvu,” anasema Kinana.
Katika mashina mengi ya wakereketwa, Kinana aliahidi fedha, vifaa ili miradi yao iweze kufanikiwa
Moja ya miradi ambayo mashina ya wakereketwa wengi walionyesha kuvutiwa nayo ni mradi wa pikipiki, maarufu kama bodaboda.
Katika ziara hiyo, wananchi mbalimbali wakiwamo viongozi walitangaza kujitoa katika vyama vya upinzani na kujiunga na CCM.
Miongoni mwao ni Mwenyekiti wa Chadema katika Kata ya Kiroka, Shaaban Mponda na Mwenyekiti wa CUF wa kata hiyo, Adimu Omar ambao walimkabidhi Kinana kadi zao.
Viongozi hao baada ya kujiunga na CCM wamesema wataendelea kuwahamasisha wanachama wa vyama vya upinzani kujiunga na CCM
Mponda anasema kuwa amekuwa akiwahamasisha wana Chadema kujiunga na chama hicho.
“Nilikuwa najitolea kusafiri kwa baiskeli kwenda vijijini kuingiza wanachama wapya, hawa nitawahamasisha kujiunga na CCM,” anasema Mponda.
Akitaja sababu ya kujiunga na CCM, Mponda anasema ni kukosa pongezi kutoka kwa viongozi wa chama hicho kikuu cha upinzani, baada ya kufanikisha kupata kijiji kuwa chini yake na vitongoji saba.
“Hakuna hata kiongozi mmoja wa Chadema aliyewahi kutembelea kata hii, hawajapata dhamana ya kuchukua nchi wako hivi, je, wakichukua watatuthamini kweli,” anahoji Mponda.
Migogoro ya ardhi
Changamoto nyingi zilizojitokeza katika ziara hiyo ni migogoro ya ardhi. Katika maeneo mengi wananchi walilalamikia ardhi kubwa kuchukuliwa na watu wachache na wananchi kuhangaika kupata mashamba.
Katibu wa Halmashauri Kuu, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye anasema tatizo hili ni la kitaifa na kwamba ni lazima sasa ifike mahali hatua za haraka zichukuliwe.
“Unakuta mtu anayejiita mwekezaji anakwenda kijijini anachukua sehemu kubwa ya ardhi na kuwaacha wananchi wakiwa hawana sehemu za kuendesha kilimo, hili tutalishughulikia kama chama,” anasema.
Tatizo jingine ambalo ni la muda mrefu katika mkoa huo ni migogoro kati ya wakulima na wafugaji.
Migogoro hiyo licha ya kudumu kwa muda mrefu lakini imendelea kutokea hali ambayo wananchi wamekuwa wakilalamikia.
Wakulima wameonyesha kukerwa na vitendo vya wafugaji kulisha mifugo yao kwenye mazao yao, hali ambayo walisema isipodhibitiwa itasababisha vurugu.
Wakulima wa miwa
Uchumi katika mji wa Turiani Madizini katika Wilaya ya Mvomero umeanza kuitafuna CCM baada ya wakulima wa miwa kutangaza vita dhidi ya kiwanda cha sukari cha Mtibwa.
Wakulima hao wanadai kuwa kiwanda hicho, kinawanyonya kwa kuwapunja fedha za ununuzi wa miwa na kuchelewesha fedha zao.
Wananchi wanadiriki kueleza wazi kwamba hata kata ya Mtibwa ambayo iko jirani na kiwanda hicho ilichukuliwa na Chadema badala ya CCM kwa sababu ya dhuluma ya mwekezaji huyo.
Wana-CCM walimweleza Kinana kwamba watu hawakuchagua chama hicho kwa sababu kilishindwa kutetea wakulima wanaouza miwa yao kwenye kiwanda hicho.
Hivyo wakaona adhabu pekee wanayoweza kuitoa ni kuchagua chama cha upinzani ili CCM ijifunze kushughulikia kero za wananchi hao.
“Viongozi wengi wa Serikali walikuja Mvomero lakini mgogoro haukumalizwa, wananchi wengi walianza kusema huenda kiwanda hiki kinamilikiwa na kigogo wa Serikali, ndiyo maana hatua hazichukuliwi,” anasema mmoja wa wana CCM kwenye mkutano na Kinana.
Wananchi hao wameomba chama kishughulikie mgogoro huo kabla `sumu’ haijapandikizwa kwenye kata nyingine.
Katika kujitetea mbele ya uongozi wa CCM, Mwakilisha wa kiwanda cha Sukari Mtibwa, Yahya Hamad amesema kucheleweshwa kwa malipo ya miwa kunatokana na ukosefu wa soko la sukari.
Anasema baada ya Serikali kuruhusu uingizwaji wa sukari kutoka nje ya nchi na kusamehe ushuru, sukari nyingi iliingizwa na kuuzwa kwa bei ya chini.
Anasema kutokana na hali hiyo bidhaa hiyo ‘ilidoda’ kiwandani na hivyo kukosa hata fedha za kuwalipa wakulima.
“Tunaomba Serikali isiruhusu sukari kuingizwa bila kulipiwa ushuru ili kulinda viwanda vya ndani,” anasema Yahya.
Kufuatia mgogoro huo, Kinana ameamuru pande tatu za mgogoro huo ambazo ni wakulima wa miwa, uongozi wa kiwanda cha Mtibwa na Halmashauri ya wilaya ya Mvomero kukutana ili kuutafutia ufumbuzi.
CHANZO: Mwananchi

0 maoni:

Chapisha Maoni

Share

Twitter Delicious Facebook Digg Stumbleupon Favorites More